WACHIMBAJI na wayeyushaji wa madini ya dhahabu katika kijiji cha Endagemu maarufu kama Samunge wameaswa kutojihusisha na utoroshaji wa madini kwa sababu kufanya hivyo kunasababisha serikali kukosa mapato na takwimu sahihi zinazopatikana katika machimbo hayo ya Madini.
Hayo yamesemwa na Mkuu wa wilaya ya Karatu Abbas Kayanda alipotembelea machimbo ya madini pamoja timu ya wataalamu wa madini na kamati ya ulinzi na usalama ya wilaya ya Karatu. Katika zaira hiyo Mkuu wa wilaya ya Karatu alipata nafasi ya kusikiliza kero za wachimbaji wa madini.
kayanda amesema shughuli za kuyeyusha dhahabu zinatakiwa kufanyika katika eneo la soko husika la madini ya dhahabu. Ametoa maelekezo kwa watendaji kuchukua hatua za kisheria kwa mtu yeyote atakayebainika kujihusisha na utoroshaji wa madini.
Pia Kayanda ametembelea eneo la chanzo cha maji lilopo Katika kitongoji cha Duum katika kijiji cha Kambi ya Faru ambalo nalo shughuli za uchimbaji wa madini zianafanyika karibu na eneo la chanzo cha maji.
Kayanda amesema sheria za mazingira zinakataza shughuli zozote za kibinadamu kufanyika ndani ya chanzo cha maji ndani ya umbali wa mita 60 kutoka chanzo cha maji kilipo. Ameongeza kusema sheria za uchimbaji wa madini zinakataza kufanyika kwa shughuli zozote za uchimbaji wa madini ndani ya mita 100 kutoka eneo la chanzo cha maji.
Akizungumzia juu ya adha ya upatikanaji maji katika ziara hiyo Mhandishi wa Ruwasa Injinia Daud Ngoitanire amesema tayari ofisi yake imeshafanya utafiti wa mwanzo na wataweka katika bajeti ya fedha ya mwaka ujao (2021-22) ili waweze kuchimba bwawa la maji katika eneo hilo ambalo litasaidia kukabiliana na changamoto ya ukosefu wa maji katika eneo la machimbo ya dhahabu Samunge.
Kwa upande wake Mhandisi wa barabara wa TARURA wa Wilaya Mchele amesema changamoto za ubovu wa barabara, tayari wameshafanya uchambuzi yakinifu wa ujenzi wa barabara na swala la ujenzi wa barabara kuelekea katika machimbo hayo litawekwa katika bajeti ya barabara ya mwaka (2021-22.)
Kuhusu nishati ya umeme ambayo ni moja ya changamoto kwa wachimbaji hao Mhandisi wa TANESCO amesema wanampango wa kufikisha huduma za umeme katika kijiji cha Endagemu na eneo la uchimbaji litakuwa eneo lengwa.
Mafunzo ya Ufugaji Bora na Matibabu, Jiunge sasa kwa KUBOFYA HAPA
Post a Comment