Mwandishi Wetu
Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA) imekabidhi vifaa mbalimbali vya afya kwa ajili ya Hospital ya Kivule iliyopo katika wilaya ya Ilala Jijini Dar es Salaam, ikiwa ni sehemu ya ushiriki wa TAA katika wiki ya maadhimisho ya Utumishi wa Umma.
Akikabidhi vifaa hivyo kwa Uongozi wa Hospitali (Jana) kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), Mkuu wa Kitengo cha Sheria na Uhusiano wa Mamlaka hiyo, Bi Pamela Mugarula alisema msaada huo umetolewa ukiwa na lengo la kumsaidia mama na mtoto.
Alisema, "Kwa kidogo ambacho tulichokipata tumeamua tukitumie kuwavusha hawa wakina mama na watoto wachanga kwani ikumbukwe kuwa Serikali mwaka 2018 ilizindua kampeni ambayo ilikuwa na lengo la kupunguza vifo vilivyotokana na uzazi na kuhakikisha mama na mtoto wanakuwa salama.
Alisema, "Katika maadhimisho haya ya Wiki ya Utumishi wa Umma, Mamlaka imeamua kujisogeza karibu na jamii iliyo karibu na viwanja vyetu vya ndege, na ndio maana tukachagua Kivule ambapo kuna hospitali kubwabaada ya kusikia Kivule ina hospitali kubwa hivyo tukaona wanastahili kupata msaada huu ili kupunguza japo kidogo baadhi ya vifaa watakavyovihitaji katika hospital hiyo."
Katika maadhimisho hayo ya Wiki ya Utumishi wa Umma ambayo uanza tarehe 16 mpaka 23 mwezi Juni kila mwaka, Mamlaka hiyo ujikita katika kusaidia jamii mbalimbali kwa kutoa msaada wa vifaa mbalimbali kama; mashuka, barakoa, dawa za kusafishia vyoo, vifaa vya Ofisi, Gloves, Vitakasa mikono, mashine za kuhifadhi vitakasa mikono, mafagio na sabuni za kunawa mikono.
Kiongozi huyo alisema kuwa msaada huu kila mwaka na mwaka huu umelenga kusaidia hospitali haswa katika huduma zinazotolewa kwa mama na mtoto ili waweze kujikinga na maambukizi mbalimbali na kwamba wataendelea kutoka msaada huo kadri itakavyowezekana.
Awali akitoa taarifa ya hospitali hiyo Mganga Mfawidhi, Dkt Thobias Nyamboto alisema hospitali hiyo inahudumia wakazi wapatao 700,000 wa Manispaa ya Ilala na Wilaya za jirani za Temeke na Kisarawe.
"Hospitali hii imeanza kutoa huduma Juni 2020 na kwasasa inahudumia wagonjwa wapatao 150 kwa siku ikiwemo wajawazito 50 na tangu kuanza kwa hospitali hii imeweza kuhudumia wagonjwa takribani elfu 24 na wajawazito 708 waliojifungua," alisema Dkt Nyamboto.
Pia ameeleza mpaka sasa kumekuwa na ongezeko kubwa la wagonjwa na wajawazito wanaojifungua kutoka maeneo mbalimbali yaliyo karibu na hospitali hiyo.
Akieleza kuhusu changamoto za hospitali hiyo, Dkt Nyamboto alisema hospitali ina changamoto ya kukosekana kwa vifaa tiba mbalimbali vya uchunguzi kama vile mashine ya mionzi (xray).
Aidha alisema kwasasa wanafanya juhudi kuhakikisha hospitali inaanza ujenzi wa wodi ya wanawake, wanaume na watoto na majengo ya afya ya kinywa na macho.
Naye Muuguzi Mkuu wa Jiji la Dar es Salaam, Bi Gerelada Mumba alisema msaada uliotolewa na TAA utatumiwa kiusahihi ili kuwahakikisha usalama mama na mtoto dhidi ya maambukizi mbalimbali hivyo wanaamini msaada huu utakuwa endelevu.
Baadhi ya Watendaji wa Mamlaka ya Viwanja vya ndege wakimsikiliza Mganga mfawidhi wa hospitali ya Kivule Dkt. Thobias Nyamboto wakati alipokuwa akionyesha majengo mapya katika hospitali hiyo wakati wa ziara ya kwenda kutoa msaada katika Hospitali ya Kivule iliyopo Wilaya ilala Jijini Dar es salaam mapema.
Watendaji kutoka Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania wakiwa kwenye picha ya pamoja na viongozi wa Hospitali ya Kivule na Halmashauri ya Jiji la Dar Es Salaam mara baada ya kukabidhi msaada katika Hospitali hiyo iliyopo Wilaya ilala Jijini Dar es salaam.
Watendaji kutoka Mamlaka ya Viwanja vya Ndege wakimsikiliza Mganga mfawidhi wa hospitali ya Kivule Dkt. Thobias Nyamboto (alienyoosha mkono) alipokuwa akionyesha ujenzi unaoendelea katika hospitali hiyo wakati wa ziara ya kwenda kutoa msaada katika Hospitali ya Kivule iliyopo Wilaya ya Ilala Jijini Dar es salaam mapema.
Mafunzo ya Ufugaji Bora na Matibabu, Jiunge sasa kwa KUBOFYA HAPA
Post a Comment