Diwani wa Kata ya Kijichi halmashauri ya Manispaa wa Temeke kupitia tiketi ya Chama cha Mapinduzi (CCM), Elias Mtarawanje (29) akiingia katika mahakama hiyo leo jijini Dar es Salaam.
DIWANI wa Kata ya Kijichi halmashauri ya Manispaa wa Temeke kupitia tiketi ya Chama cha Mapinduzi (CCM), Elias Mtarawanje (29), amefikishwa katika Mahakama ya Wilaya ya Temeke akikabiliwa na mashtaka mawili likiwamo la kupokea rushwa ya Sh. Milioni moja kutoka kwa Yusuf Omary.
Diwani huyo amefikishwa mahakamani hapo leo Mei 21, 2020 mbele ya Hakimu Mkazi Catherine Madili.
Akisoma hati ya mashtaka mwendesha mashtaka kutoka Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), Mwanakombo Rajabu amedai Februari 6, mwaka huu katika eneo la Mtoni Kijichi lililopo Temeke jijini Dar es Salaam mshtakiwa huyo akiwa kama Diwani wa Kijichi aliomba rushwa ya Sh. Milioni moja kutoka kwa Yusuf Omary kama kishawishi kwake ili asiweze kuzuia malipo ya fidia la eneo jambo ambalo amelifanya tofauti na mahusiano ya shughuli za mwajiri wake.
Katika shtaka la pili, imedaiwa kuwa Februari 6, mwaka huu, eneo hilo hilo la Mtoni Kijichi mshtakiwa huyo akiwa diwani kwa njia za rushwa alijipatia Sh. Milioni moja kama kishawishi kwake ili asiweze kuzuia malipo ya fidia ya eneo jambo ambalo amelifanya tofauti na mahusiano ya shughuli za mwajiri wake.
Hata hivyo, mshtakiwa amekana kutenda makosa hayo, upande wa Takukuru ulidai kuwa upelelezi wa shauri hilo umekamilika hivyo wanaomba tarehe kwa ajili ya mshtakiwa kusomewa maelezo ya awali.
Akitoa masharti ya dhamana, Hakimu Madili alimtaka mshtakiwa kuwa na wadhamini wawili watakaosaini bodi ya sh. 500,000 kila mmoja.
Mshtakiwa amefanikiwa kutimiza masharti ameachiwa kwa dhamana, na kesi imeharishwa hadi Juni 3, 2020.
Mafunzo ya Ufugaji Bora na Matibabu, Jiunge sasa kwa KUBOFYA HAPA
Post a Comment