PINDA AWAAGIZA WABUNGE NA MADIWANI WA CCM KUTATUA KERO ZA WANANCHI | Tarimo Blog

Na Denis Mlowe, Iringa

WAZIRI MKUU Mstaafu na Mlezi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Iringa Mizengo Pinda amewaagiza viongozi katika ngazi mbalimbali mkoani Iringa ambao walichaguliwa kwa tiketi ya chama hicho kwenye Uchaguzi Mkuu uliopita kwenda kuisimamia Ilani kwa kushughulikia changamoto za wananchi waliowachagua.

Akizungumza katika Semina Elekezi iliyohusisha wabunge wote na madiwani wote wa CCM Mkoa wa Iringa na kufanyika katika ukumbi wa CCM mkoa wa Iringa, Mizengo Pinda alisema imani ambayo wananchi wamekionyesha chama hicho kwenye Uchaguzi Mkuu na kuwapa ushindi mkubwa ni kubwa na ina stahili kulipwa kwa kuwatumikia wananchi kama ambavyo imeainishwa kwenye Ilani ya chama.

Alisema kuwa wananchi wamekipa imani chama cha Mapinduzi na sasa ni zamu ya waliochaguliwa kuwaletea maendeleo ambayo wananchi wanayasubiri kwa hamu kubwa na ikumbukwe kwamba mbunge au diwani ambaye hatafanya kazi kwa misingi ilani ya chama katika kuwaletea maendeleo wananchi anawapa kazi kubwa chama kuweza kushinda katika chaguzi zake.

Aidha Pinda alisema kuwa chama kinatakiwa kutembelea miradi yote ambayo serikali inatekeleza kwenye maeneo ya wananchi kwani usipofanya hivyo huko kwenye kata wananchi kuna malalamiko mengi na unakuta diwani hata kwenye mradi mmoja hajafika hapo utakuwa diwani wa ajabu sana.

"Lazima twende kutembelea miradi kuona ile ilani ambayo wananchi walielezwa kwenye kampeni inakwenda  inavyotakiwa? tukifanya hayo ndugu zangu tutaona sehemu kubwa kabisa tutafanya kazi ya chama kuwa nyepesi na kurahisha shughuli katika chaguzi zinazofata."  Alisema

Aliongeza kuwa wabunge au madiwani kufanya ziara kwenye maeneo yao ni lazima isitokee kiongozi anasema kuwa asipangiwe shughuli za kufanya kumbuka chama kina taratibu zake na chama kikiona hufanyi kazi vizuri hakiwezi kukuacha hivi hivi kwani lazima chama kimbane mbunge kuhakikisha anafanya ziara kwenda kusikiliza changamoto za watu ,kuyapatia ufumbuzi na aweke utaratibu wa kusikiliza kero za watu kila wiki au kila anapopata muda.

Alisema kuwa kama mbunge au diwani hafanyi kazi yake ipasavyo ndio chanzo cha rais Magufuli kufikishiwa barua nyingi ambazo hazina sababu kwa sababu wa chini yake hawafanyi kazi ipasavyo hivyo ni wajibu wa kila mbunge na diwani kufanya hivyo kusikiliza kero za wananchi.

Alisema kuwa ukifanya wajibu wako wa kukutana na makundi ambayo yamesaidia kwa kiasi kikubwa kufanikisha ushindi na kusikiliza kero zao na sio kama ilivyo kuwatafuta kipindi cha uchaguzi kisha wakati huku mwanzo ulikaa kimya hiyo safari hii kama chama hakiwezi kuvumilia.

Pinda alitoa wito kwa viongozi kuhakikisha sekta binafsi kutoiweka pembeni katika maendeleo ya nchi hivyo ndani ya chama tawala tuone namna gani sekta binafsi inapata nafasi ya kusikilizwa kila mara kwa lengo la kuona changamoto wanazokabiliana nazo ili kuziondoa.

Aidha alitoa wito kwa viongozi kuhakikisha wanasoma ilani kwa umakini ili kuweza kubaini ahadi za wananchi katika kuwaletea maendeleo hivyo wananchi wanategemea mengi kutoka ndani ya chama cha Mapinduzi walichokipa madaraka ya kuongoza dora.

akizungumzia kuhusu mapato ya chama Pinda alisema kuwa bado inahitajika nguvu kubwa katika kukiletea mapato chama kwani inahitajika kazi kubwa na kuwataka makatibu kusimamia makusanyo ya mapato kila mkoa ili kukifanya chama kiweze kujitegemea iwe ajenda ya watu wote wakiwemo wabunge na madiwani kiwe kinajitegemea.

Aliwataka kuhakikisha miradi iliyopo inasimamiwa vizuri kila kinachopatikana kiende kikafanye kazi ya kujenga chama hivyo wale wenye tabia ya kukusanya fedha na kuingia mfukoni waache mara moja kwani hadi majuzi hapa kuna taarifa kuna baadhi wanakula fedha za chama hivyo lazima kuwe na miradi katika ngazi ya kata, ngazi ya tawi lazima hata kama midogo itasaidia.

Aidha alisema kuwa mafunzo kwa viongozi na makada ni muhimu sana yanasaidia kukumbushana mambo mbalimbali ya uongozi kuliko kukaa bila mafunzo na kuwaacha viongozi kutoelewa suala zima la kuongoza.

Kwa upande wake Mwenyekit wa CCM Mkoa wa Iringa Dk Abel Nyamahanga alisema wao kama chama watapita katika maeneo mbalimbali kuangalia utekelezaji wa ilani na kamwe hawatakuwa na simile na kiongozi atakayeshindwa kutekeleza kwa vitendo ahadi alizozitoa kwa wananchi kipindi cha uchaguzi.

Kwa upande wao baadhi ya wabunge akiwemo Justin Nyamoga Mbunge wa jimbo la Kilolo alisema kuwa maagizo waliyopewa na watayafanyia kazi kwa lengo la kuwaletea maendeleo wananchi na kuhakikisha ahadi zote zinafanyiwa kazi.

Nyamoga alisema kuwa semina hiyo imewejenga kwa kiasi kikubwa kwani inawakumbusha kwamba wale wote waliochaguliwa wana deni kubwa kwa wananchi na endapo wakizembea katika kuwatumikia wananchi kutakuwa na kazi kubwa sana katika chaguzi zijazo,

"wananchi wametupa imani kubwa sana na ndio maana tukaibuka na ushindi wa kishindo katika chaguzi iliyopita hivyo deni hili linalipwa kwa kuwaletea maendeleo wananchi waliotuchagua na kumpa kura za kishindo rais Magufuli" alisema...


Waziri Mkuu mstaafu Mizengo Pinda akisalimiana na madiwani na wabunge wa Ccm mkoa wa Iringa wakati wa semina elekezi.
Mwenyekiti wa Ccm mkoa wa Iringa Abel Nyamahanga akizungumza kwenye Semina hiyo



Mafunzo ya Ufugaji Bora na Matibabu, Jiunge sasa kwa KUBOFYA HAPA

0/Post a Comment/Comments

Previous Post Next Post

Ad

Ads1

Sponsor Ad

Ads2