TGDC YAJIPANGA KUZALALISHA UMEME, KUFUNGUA FURSA MATUMIZI NISHATI JOTOARDHI | Tarimo Blog

 

Meneja Mkuu wa Kampuni wa Uendelezaji Jotoardhi (TGDC) Tanzania Mhandisi Kato Kabaka akiwasilisha mada kuhusu shughuli zinazofanywa na TGDC katika kikao kazi cha wahariri waandamizi wa vyombo vya habari (hawapo pichani) nchini kinachofanyika mjini Morogoro.
Baadhi washirika wa kikao kazi cha wahariri waandamizi wa vyombo vya habari nchini kinachofanyika mjini Morogoro.
Meneja Mkuu wa Kampuni wa Uendelezaji Jotoardhi (TGDC) Tanzania Mhandisi Kato Kabaka akitolea ufafanuzi maswali yaliyoulizwa katika kikao kazi cha wahariri waandamizi wa vyombo vya habari nchini.


Na Said Mwishehe, Michuzi TV-Morogoro

MENEJA Mkuu wa Kampuni wa Uendelezaji Jotoardhi (TGDC) Tanzania Mhandisi Kato Kabaka amesema kuwa TGDC inapanga kuzalisha umeme na kufungua fursa za matumizi ya nishati ya jotoardhi katika ukuaji wa uchumi wa nchini.

Akizungumza mjini Morogoro katika kikao kazi cha Wahariri waandamizi wa vyombo vya habari nchini amesema Serikali kupitia TGDC inaendelea na miradi ya kimkakati ya uendelezaji wa nishati ya jotoardhi kufukia lengo la serikali la uzalishaji wa megawati 200 kufikia mwaka 2025.

"Miradi ya kipaumbele TGDC ni mradi wa Ngozi Mkoa wa Mbeya, Songwe Mkoa wa Songwe, Kiejo Mbaka Mkoa wa Mbeya, Natron Mkoa wa Arusha na Luhoi Mkoa wa Pwani huku miradi yote ikilenga kuzalisha megawati 200," amesema Mhandisi Kabaka.

Ameongeza shughuli za utafiti wa kina wa nishati wa jotoardhi katika miradi ya kipaumbele  ya kuzalisha umeme zinaendelea na kwa sasa TGDC imefikia hatua ya uchorongaji visima vya jotoardhi ili kuhakiki kiwango cha hifadhi halisi ya jotoardhi iliyoko chini ya ardhi.

"Katika muendelezo wa tafiti za kina siku chache zijazo TGDC inakusudia kusaini mkataba na mkandarasi wa ndani  ya nchi ili kutekeleza mradi wa uchorongaji visima vifupi vya utafiti vya nishati ya jotoardhi katika Mradi wetu wa Kiejo - Mbaka eneo la Halmashauri ya Busokelo Wilaya ya Rungwe Mkoani Mbeya,"amefafanua.

Mhandisi Kabaka amesema katika utekelezaji wa miradi TGDC inatekeleza miradi yake sambamba na mipango na sera ya serikali, ili kuhakikisha nishati ya jotoardhi inafungamanishwa na shughuli nyingine za uchumi nchini.

"Sekta ambazo tunapanga kufungamanisha nazo katika uendelezaji wa rasilimali ya jotoardhi nchini ni pamoja na sekta ya nishati, kilimo, ufugaji, viwanda, biashara na utalii,"amesema.

Aidha, Mhandisi Kabaka ameongeza kwa sasa pamoja na TGDC kuendelea na jitihada za uendelezaji wa nishati ya jotoardhi katika uzalishaji wa umeme tayari kuna fursa zimebuniwa na TGDC zikiwa na lengo la kuchangia katika shughuli za kiuchumi nchini.

"Fursa hizi ni matumizi ya rasiliamali ya jotoardhi yanayopatikana katika Mradi wa Songwe Mkoani Songwe kutumia rasilimali ya jotoardhi kutotolesha vifaranga,  kufugia samaki, kilimo, ushughuli za utalii na shughuli nyingine,"amesema.


Mafunzo ya Ufugaji Bora na Matibabu, Jiunge sasa kwa KUBOFYA HAPA

0/Post a Comment/Comments

Previous Post Next Post

Ad

Ads1

Sponsor Ad

Ads2