'MC' WA RAIS MAGUFULI AFUNGUKA NAMNA ALIVYOMFAHAMU ' ALIKUA KIONGOZI WA KUTUMAINIWA' | Tarimo Blog


Charles James, Michuzi TV

ALIKUA Kiongozi wa kutumainiwa! Ni kauli ya Mwenyekiti wa Wazee wa Chama cha Mapinduzi Mkoa wa Dodoma, Peter Mavunde akimuelezea Rais Dk John Magufuli ambaye amefariki Dunia na kuacha simanzi kwa watanzania.

Michuzi Blog imezungumza na Mzee Mavunde katika mahojiano maalum hii leo jijini Dodoma ambapo amemuelezea Rais Dk John Magufuli kama kiongozi mchapakazi, aliyependa haki na mwenye uzalendo usio na hata chembe ya doa.

Mzee Mavunde ambaye pia mara kwa mara alikua mshereheshaji 'MC' katika matukio yaliyomuhusu Rais Magufuli amesema kwa muda wote aliomfahamu alimuona kama kiongozi aliyechukia rushwa kwa dhati huku akiwapenda watanzania na akichukia uzembe kazini na alipambana na maovu yote bila woga.

Amesema Rais Dk Magufuli alisimamia sheria siyo tu alivyokua Rais bali hata kipindi akiwa Waziri katika Serikali ya awamu ya tatu chini ya Rais Benjamin Mkapa na Serikali ya awamu ya nne iliyoongozwa na Rais Jakaya Kikwete na daima alionesha ujasiri wake katika kuwatumikia watanzania.

" Kwetu sisi Watanzania huu ni msiba mkubwa na Msiba wa kwanza kwa watanzania kushuhudia Rais wetu akiwa madarakani akiondoka na kutuacha kwani tulikua na mategemeo makubwa sana kuona kwamba ndoto na kiu ya hayati Rais Magufuli zinatimia na yeye akiona alichotuahidi ametekeleza, lakini sisi hatuwezi kupingana na mapenzi ya Mwenyezi Mungu.

Watanzania tulimtegemea Rais Magufuli, tulimpenda, tulimuamini na tulikua na shauku ya kuona akituvusha kwenye mambo mbalimbali, tumeona ununuzi wa Ndege, ujenzi wa Reli ya Mwendokasi unaoendelea sasa, Bwawa la Umeme la Mwalimu Nyerere ambalo limezaa Hifadhi ya Taifa ya Mwalimu Nyerere na miradi mikubwa mingi tena akiyafanya kwa kipindi kifupi sasa, kwa hayo yote tuna deni kwake katika kuyaenzi na kuyaendeleza," Amesema Mzee Mavunde.

Mzee Mavunde amesema katika kumuenzi Rais Magufuli watanzania wanapaswa kushikamana na viongozi wengine ambao wataletwa na Mwenyezi Mungu katika kuyaendeleza yale yote makubwa aliyoyaanzisha ili kuweza kufikia maendeleo makubwa ambayo Rais Magufuli aliyaanzisha.

Pimia amemshukuru Rais Magufuli kwa namna ambavyo aliupa Mkoa wa Dodoma kipaumbele kwenye muda wake wa uongozi ikiwa ni pamoja na kupitisha sheria ya Dodoma kuwa Makao Makuu ya Nchi lakini pia akiupa hadhi Mji wa Dodoma kuwa Jiji jambo ambalo anaamini litamfanya azidi kukumbukwa na wana-Dodoma kwa miaka yote na akiishi mioyoni mwao.

" Mimi nimekua mkazi wa Dodoma kuanzia mwaka 1971 hivyo nina miaka 49 nimehudumu pale CDA kabla haijavunjwa nilishuhudia Dodoma ikitangazwa makao makuu mwaka 1973 tulifanya kazi nyingi chini ya Mwalimu Nyerere kuanzia kwenye master plan ya Mji mpaka ukathibitishwa lakini vita ya Uganda ikafanya mchakato ukadorora.

Alipoingia Rais Magufuli hatukujua kama atatangaza Dodoma kuwa Jiji lakini alitangaza Dodoma kuwa Makao Makuu na Dodoma kuwa Jiji hii ni zawadi ambayo haitofutika mioyoni mwetu, tutasimama Kidete katika kumuenzi Rais wetu kwani ametufanyia jambo kubwa lenye kutuheshimisha na leo tunazungumzwa na kuwa na hadhi kubwa kwa sababu ya Rais wetu," Amesema Mzee Mavunde.

Amesema kwa maendeleo makubwa yaliyofanywa na Rais Magufuli ndani ya Dodoma wana deni kubwa sana la kuenzi mambo yote yaliyofanywa na serikali yake kwani licha ya kuhamishiwa Makao Makuu ya Nchi na Serikali Dodoma lakini ameleta na maendeleo pia.


 

Mafunzo ya Ufugaji Bora na Matibabu, Jiunge sasa kwa KUBOFYA HAPA

1/Post a Comment/Comments

Post a Comment

Previous Post Next Post

Ad

Ads1

Sponsor Ad

Ads2