TUNALINDA JAMII NA MAZINGIRA DHIDI YA ATHARI ZA MIONZI - TAEC | Tarimo Blog



Waziri wa Elimu Sayansi na Teknolojia, Profesa Joyce Ndalichako akifungua semina ya wahariri wa vyombo vya Habari na waandishi wa habari iliyoandaliwa na Tume ya Nguvu za Atomiki (TAEC) inayofanyika kwenye ukumbi wa Jengo la Utawala la Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM)  Semina iliyofanyika mwishoni mwa wiki.

Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu Cha Dar es Salaam,  Profesa William Anangisye akitoa ukaribisho kwa Waziri, Tume ya Nguvu za Atomiki  (TAEC)na washiriki wa semina ya kutoa mafunzo kwa wahariri na waandishi wa vyombo vya habari yaliyofanyika UDSM. Alisemakuwa kwa mwaka wa masomo 2020/2021 Chuo kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) kimedahili wanafunzi 60 wanaosoma kozi inayohusiana na nguvu za atomiki huku kukiwepo na wanafunzi 7 wanaosoma shahada ya umahiri kuhusu masuala ya nguvu za atomiki.
Waziri wa Elimu Sayansi na Teknolojia, Profesa Joyce Ndalichako, Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Willium Anangisye na Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Nguvu za Atomiki Tanzania (TAEC,) Prof. Lazaro Busagala, wahariri na waandishi wa habari  wa wakiwa katika picha ya pamoja.
Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Nguvu za Atomiki (TAEC) Profesa Lazaro Busagala akizungumza katika semina kwa wahariri na waandishi wa habari ili kuwajengea uwezo na udhibiti na matumizi salama ya mionzi  nchini pamoja na kuwajengea uelewa  kuhusu Jukumu la (TAEC) kwa Taifa na jamii kwa ujumla. Semina hiyo ilifanyika katika ukumbi wa jengo la utawala Chuo Kikuu Cha Dar es Salaam (UDSM) mwishoni mwa wiki.

Mkuu wa Ofisi ya Kanda ya Dar es Salaam Tume ya Unguvu za Atomiki (TAEC,) Dkt. Wilbroard Muhogora akiwasilisha mada kuhusu mionzi katika semina ya wahariri na waandishi  wa habari katika semina iliyofanyika katika ukumbi uliopo katika jengo la utawala Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.
Mtafiti Mwandamizi Sayansi ya Nyukilia, Alex Pius Muhulo akiwasilisha mada kuhusu mionzi katika matibabu na utafiti wa magonjwa kwa binadamu.


Leandra Gabriel  na Avila Kakingo - Michuzi TV

 KATIKA kuhakikisha jamii inaelewa zaidi juu ya majukumu yanayotekelezwa na Tume ya Nguvu za Atomiki Tanzania (TAEC,) tume hiyo imekutana na kutoa semina ya kitaifa kwa wahariri na waandishi wa habari Mkoani Dar es Salaam  kuhusu nguvu za atomiki, matumizi yake pamoja na tahadhari zinazopaswa kuchukuliwa na jamii kwa ujumla.

Akizungumza wakati wa semina hiyo Mkuu wa ofisini ya (TAEC,) kanda ya Dar es Salaam Dkt. Wilbroard Muhogora ameeleza namna tume hiyo inavyolinda watu na mazingira katika kuhakikisha hawaathiriki na mionzi na wamekuwa wakipima sampuli 9400 za vyakula ndani ya miezi mitatu chini ya wataalamu wapatao 1942 nchi nzima.

Amesema, Tume hiyo imekuwa ikidhibiti matumizi salama ya mionzi ili kulinda Umma, wafanyakazi na mazingira dhidi ya madhara ya mionzi  pamoja na kuhamasisha matumizi salama ya teknolojia ya nyuklia kwa maendeleo endelevu ya jamii na uchumi.

Katika kuhakikisha usalama kwa jamii dhidi mionzi Muhogora amesema, Tume imekuwa ikifanya ufuatiliaji wa mara kwa mara wa viashiria vya mionzi katika vyakula vinavyoingizwa ndani ya nchi kuhakikisha kuwa ni salama kwa matumizi ya binadamu.

"Kwa upande wa mazingira tume hufuatilia viasilia vya mionzi katika madini, makaa ya mawe, fosfeti, mbolea pamoja na  vifaa vya ujenzi pia tume hufanya uchambuzi mionzi kwa sampuli zote zinazoletwa na wateja na baadaye kutoa vibali vya kuthibitisha ubora wa sampuli hizo." Amesema.

Awali akifafanua kuhusu dhana ya mionzi Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Nguvu za Atomiki Tanzania Prof. Lazaro Busagala amesema jamii imekuwa ikihusianisha dhana ya mionzi/ nguvu za atomiki na mabomu jambo ambalo siyo sahihi na kueleza kuwa, mionzi ina faida nyingi kwa maendeleo na ustawi wa katika jamii na hutumika katika sekta mbalimbali ikiwemo afya, elimu, kilimo, mifugo na viwanda na kusisitiza kuwa isipotumika kwa usahihi inaweza kuingia katika mnyororo wa chakula ambao ni hatari kwa afya ya binadamu na wanyama.

Akifungua mafunzo hayo Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako alisema kuwa matumizi sahihi ya nguvu za atomiki zimekuwa zikinufaisha sekta mbalimbali ikiwemo elimu, afya, mafuta, gesi, kilimo, mifugo na viwanda.

Prof. Ndalichako aliishauri jamii kufatilia taarifa zinazotolewa na tume hiyo ili kufahamu faida na tahadhari zinazotolewa ili kuweza kujiepusha na mionzi hatarishi.

Pia aliwataka waandishi wa habari kuendelea kutumia vyema kalamu zao katika kuhabarisha jamii kwa namna ya kujenga jamii imara.


Mafunzo ya Ufugaji Bora na Matibabu, Jiunge sasa kwa KUBOFYA HAPA

0/Post a Comment/Comments

Previous Post Next Post

Ad

Ads1

Sponsor Ad

Ads2