DC NTEMO APIGA STOP MADANGURO MSANGANI, ATAKAEBAINIKA KUKIONA | Tarimo Blog

 

Na Mwamvua Mwinyi,Kibaha
MKUU wa wilaya ya Kibaha, Mhandisi Martin Ntemo amekemea vitendo vya kuendesha biashara ya ngono yaani madanguro katika kata ya Msangani na kuomba wananchi watoe taarifa za watu wanaoendeshwa madanguro pamoja na uhalifu mbalimbali .

Ntemo aliyasema hayo alipokuwa akisikiliza kero na kutatua changamoto zinazoikabili kata ya Msangani huku akiwa ameambatana na wataalamu wa kutoka Halmashauri ya Mji wa Kibaha.

Alisema kwamba, madanguro hayakubaliki ndani ya jamii kwani yanakwenda kinyume kimaadili ,yanaathiri watoto kwa vijana ambao wanajiingiza kwenye ufuska na yanaenda kinyume na mila na desturi za nchi yetu .

Alieleza, vitendo vya aina hii na uhalifu ni viovu na vya kiuhalifu vinasabisha watu washindwe kufanya shughuli za maendeleo.

“Wananchi toeni taarifa ya vitendo hivyo kwani havistahili ndani ya jamii  lazima tuvikemee kwa nguvu zote na si vya kuvifumbia macho,”alifafanua Ntemo.

Changamoto nyingine ni wakazi kutaka kumilikishwa eneo ambalo ni sehemu ya msitu wa hifadhi ya Ruvu Kaskazini ,ambapo Ntemo alielezea ,jambo hilo sio sahihi kwakuwa msitu huo ulitengwa kwa ajili ya kuchuja hewa chafu ya viwanda na ikizingatiwa Pwani ni mkoa wenye viwanda vingi .


Nae mwakilishi wa kamanda wa Polisi wilaya OCD, Michael Milinga alisema kuwa ,wameshaanza kuchukua hatua ya kuwakamata watu wanaojihusisha na madanguro hayo japokuwa baadhi wamekimbia baada ya kubainika.

Alisema, watu hao wanaendelea kutafutwa ili wachukuliwe hatua za kisheria.


Milinga alibainisha, wahusika wakuu wa madanguro hayo wanatoka nje ya Kibaha ikiwemo Gongolamboto na Ukonga Banana Jijini Dar es Salaam ambao wanaharibu hasa watoto.

Mafunzo ya Ufugaji Bora na Matibabu, Jiunge sasa kwa KUBOFYA HAPA

0/Post a Comment/Comments

Previous Post Next Post

Ad

Ads1

Sponsor Ad

Ads2